Ligi Kuu England inatarajiwa kukataa kuongeza matumizi ya VAR msimu ujao baada ya mashauriano kati ya viongozi wa ligi hiyo na chombo cha waamuzi cha PGMO. Hatua hiyo inakuja licha ya sheria mpya ya Ifab kuruhusu VAR kuamua kuhusu kona na kadi za pili za njano kuanzia mwezi ujao.
Sheria hiyo mpya itatumika katika Kombe la Dunia baada ya ombi kutoka kwa FIFA, lakini utekelezaji wake umeachwa kwa hiari ya mashindano na ligi mbalimbali. Klabu za Premier League zitatoa uamuzi wa mwisho katika mkutano mkuu wa mwaka ujao mwezi ujao, huku PGMO ikipendekeza wazi kuwa mamlaka ya VAR yasipanuliwe.
Sababu kubwa ya upinzani huo ni hofu kwamba kuongezeka kwa majukumu ya VAR kutachelewesha mechi na kuongeza usumbufu kwa mashabiki pamoja na wadau wa matangazo ya televisheni. Pia kuna wasiwasi kuwa waamuzi wataongezewa presha kubwa zaidi katika kufanya maamuzi ya haraka na sahihi.
Kwa upande mwingine, FIFA inaamini kuwa makosa madogo kama kona isiyo sahihi yanaweza kuamua hatima ya mechi kubwa za Kombe la Dunia, hasa katika hatua za mtoano. Mwenyekiti wa kamati ya waamuzi ya FIFA, Pierluigi Collina, pamoja na rais wa FIFA, Gianni Infantino, wanaunga mkono matumizi mapana ya VAR ili kupunguza makosa yenye athari kubwa.
Mjadala huo umechochewa zaidi na tukio la Jumapili ambapo mwamuzi Chris Kavanagh alimnyima Callum Wilson bao la kusawazisha dakika za mwisho dhidi ya Arsenal baada ya kushauriana na VAR, Darren England. Uamuzi huo unaweza kuwa na athari kubwa katika mbio za ubingwa pamoja na vita vya kushuka daraja.
Mkuu wa waamuzi wa PGMO, Howard Webb, anatarajiwa kuzungumzia tukio hilo katika kipindi cha Sky Sports “Match Officials Mic’d Up”, huku PGMO ikisisitiza kuwa taratibu zote zilifuatwa ipasavyo.
Wakati huo huo, Ifab pia inatarajiwa kujadili tatizo la wachezaji kushikana na kuvutana wakati wa kona, jambo ambalo limekuwa likionekana mara nyingi katika Premier League msimu huu.


Comments
Loading…