Mikel Arteta anaweza kusherehekea kumbukumbu ya miaka sita tangu ateuliwe kuwa kocha wa Arsenal akiwa kileleni mwa Ligi Kuu ya England, baada ya timu yake kujibu changamoto ya Manchester City kwa ushindi mwembamba lakini uliostahili dhidi ya Everton. Nafasi ya kuwa namba moja wakati wa Krismasi sasa imehakikishwa, ingawa Arteta atafahamu kuwa watahitaji kuboresha kiwango chao, zaidi ili kubaki hapo hadi mwisho wa msimu.
Penalti ya Viktor Gyökeres iliyopigwa kwa nguvu kipindi cha kwanza ilitosha kuipatia Arsenal ushindi muhimu ugenini dhidi ya Everton ambao ilikosa baadhi ya wachezaji wake muhimu. Uchezaji wa Arsenal ulikuwa wenye ufanisi zaidi kuliko kuvutia, wenye uimara zaidi kuliko ubabe, lakini huu ulikuwa mtihani wa tabia baada ya mechi tatu za ugenini bila ushindi kwenye Ligi, na kupoteza uongozi kwa mara ya kwanza, tangu katikati ya Oktoba muda mfupi kabla ya mchezo kuanza. Kikosi cha Arteta kilihakikisha kuwa kukaa kwa City kileleni kungekuwa kwa muda mfupi.

Hakukuwa na mengi ya kuripoti katika mwanzo wa mchezo uliokuwa wa kuchosha, zaidi ya uimbaji wa kudhalilisha na wa mara kwa mara kuhusu umaskini kutoka kwa mashabiki wa Arsenal waliokuwa ugenini. Hata hivyo, sifa ziwaendee waliamua kuonyesha tangazo la ‘Fans Supporting Foodbanks’ kwenye skrini kubwa za uwanja kama jibu.
Hatimaye, na kwa namna isiyoeleweka, Jake O’Brien aliupa mchezo uhai kwa kipindi kifupi chenye vurugu. Mlinzi wa Everton alimkumba Gyökeres wakati mshambuliaji huyo wa Arsenal alipoonekana kuwa na uhakika wa kufunga baada ya krosi ya Jurriën Timber. Gyökeres alidai penalti mara moja lakini VAR ilikagua na kukataa, ikisema hakukuwa na faulo. Mshambuliaji alihitaji kuwa imara zaidi katika mapambano hayo.
Hata hivyo, haikujalisha. Kutokana na kona iliyofuata, baada ya Vitalii Mykolenko kugusa krosi ya Timber mwisho, O’Brien alishika mpira waziwazi akiwa chini ya presha kutoka kwa Riccardo Calafiori na Piero Hincapie. Mwamuzi Sam Barrott, aliyekuwa hajaliona tukio hilo awali, alitumwa kwenye skrini ya pembeni mwa uwanja, na alipoona mchezaji wa Jamhuri ya Ireland akiinua mikono yote miwili kuelekea mpira, hakuwa na chaguo lingine ila kutoa penalti. Gyökeres aliipiga kwa nguvu na kumpita Jordan Pickford. Kasi na nguvu ya mkwaju huo vilimwacha mlinda mlango wa Everton bila nafasi, licha ya kuruka upande sahihi.
Kipindi kilichobaki cha kwanza kilirejea katika hali ya awali: kilikuwa butu. Declan Rice na Martín Zubimendi walidhibiti eneo la kati, na Arsenal walicheza kwa utulivu zaidi, lakini wao pamoja na Everton hawakutengeneza nafasi nyingi. William Saliba alimpa Gyökeres nafasi nzuri kabla ya mapumziko, lakini mshambuliaji huyo alipiga juu akiwa chini ya presha ya James Tarkowski.
Kutokuwa na makali kwa Everton hakukuwa mshangao. Bila Kiernan Dewsbury-Hall (majeruhi) na Iliman Nidiaye (aliyekuwa AFCON), David Moyes alikosa vipaji viwili muhimu na wabunifu zaidi msimu huu. Pengo la ubora kati ya wawili hao na waliowachukua nafasi yao, Carlos Alcaraz na Dwight McNeil, lilionekana wazi na liliathiri timu ya nyumbani.

Kipindi cha pili kilikuwa wazi na chenye kasi zaidi, kikileta maboresho yaliyokaribishwa. Arsenal walikaribia kuongeza bao dakika chache baada ya kuanza tena wakati Bukayo Saka na Timber walipoungana vizuri upande wa kushoto wa Everton. Baada ya kumpasia beki wake aliyepanda ndani ya boksi, Saka alifuata pasi ya kurudi iliyopimwa vyema. Shuti lake la chini lilimpita Pickford lakini likazuiwa kwenye mstari wa goli na Tarkowski.
Wageni pia waligonga mwamba mara mbili ndani ya dakika nne. Leandro Trossard alipiga shuti la mara ya kwanza lililopinda na kugonga nguzo ya mbali baada ya Rice kwa kujitoa kafara kumpasia badala ya kupiga mwenyewe. Trossard alipaswa kufunga. Zubimendi naye alipiga mpira uliogonga chini ya besela hiyohiyo kutoka kwa pasi nzuri ya kurudishwa na Martin Ødegaard kutoka mstari wa mwisho.
Everton nao walionekana kuimarika, ingawa matumaini yao makubwa ya kusawazisha yalihusu madai ya penalti. La kwanza lilikuwa dhaifu na likapuuzwa wakati Thierno Barry alianguka baada ya kuguswa na Zubimendi kufuatia pasi mbaya ya Saliba kutoka kwenye safu ya ulinzi. Dai la pili lilionekana na nguvu zaidi pale Saliba na Barry walipopigania mpira ndani ya boksi, na mlinzi wa Arsenal akamkanyaga mguu wa mshambuliaji wa Everton baada ya yeye kuuchezea mpira. VAR iliamua kuwa mguso haukuwa wa kutosha kutoa penalti.


Comments
Loading…