Arsenal wakiisambaratisha Atlético Madrid 4–0
Arsenal waliendeleza ubabe wao barani Ulaya kwa ushindi mnono wa mabao 4–0 dhidi ya Atlético Madrid kwenye Uwanja wa Emirates, katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya uliokuwa na kasi, nidhamu na ubora mkubwa wa wapinzani wote hadi dakika ya 57.
Kwa muda mrefu, kikosi cha Diego Simeone kilionekana kuwa ndani ya mchezo. Walijilinda kwa umakini, wakapiga besela kupitia Julián Álvarez, na kwa muda wakaamini wanaweza kuondoka London wakiwa na kitu. Lakini baada ya dakika ya 57, mambo yalibadilika ghafla — Arsenal wakabadili ‘Gia’ kwa kasi, tena kasi ya ukatili ulioacha wageni wakiwa hawajitambui.
Bao la kwanza lilitokana na mpira wa kona uliopigwa na Declan Rice, na Gabriel Magalhães akaurukia kwa kichwa kuwatanguliza wenyeji. Dakika chache baadaye, mchanganyiko huohuo ulizaa tena matunda — Rice akampatia Gabriel, ambaye safari hii alimpasia Viktor Gyökeres aliyesukuma mpira wavuni kwa urahisi, na kufanya matokeo kuwa 2–0.
Kati ya mabao hayo mawili, kijana Myles Lewis-Skelly alifanya kazi ya kipekee alipokimbia katikati ya uwanja na kumpa Gabriel Martinelli pasi safi, ambayo Mbrasil huyo aliimalizia kwa utulivu mkubwa akipiga shuti la chini lililompita kipa Jan Oblak.

Gyökeres, aliyekuwa akikosolewa kwa ukame wa mabao uliodumu mechi tisa, alipata faraja alipofunga tena kwa bao la tatu, mpira ukimpiga David Hancko na kumpoteza Oblak. Dakika chache baadaye, Mswidi huyo akaongeza la nne kutoka karibu, akipokea pasi ya kichwa kutoka kwa Gabriel. Mashabiki wakamshangilia kwa wimbo na makofi alipotolewa dakika za mwisho.
Atlético walijaribu kurudi mchezoni kupitia kijana Giuliano Simeone, mwana wa kocha wao, lakini mabeki wa Arsenal wakiongozwa na Gabriel na William Saliba walikuwa thabiti kama mwamba.
Kwa ushindi huu, Arsenal wamefunga mabao 4 dhidi ya wapinzani waliokuwa katika kiwango bora — Atlético wakiwa wametoka kuifunga Real Madrid 5–2 wiki iliyopita. Kikosi cha Mikel Arteta sasa kimecheza mechi 12 msimu huu bila kufungwa zaidi ya mabao matatu kwa jumla, jambo linaloonyesha uimara wao wa kiulinzi na ubora wa mfumo wao wa kushambulia.
Rice na Gabriel walitawala mipira ya kona, Martinelli akang’ara upande wa kushoto, huku Gyökeres akionyesha nguvu, kasi na ari ya kupambana — sifa zilizomfanya aonekane kama “ng’ombe wa vita” mbele ya mabeki wa Atlético.
Arteta alionekana mwenye furaha baada ya mchezo, akisema:
“Kitu cha muhimu ni ujasiri wa wachezaji wangu. Hawakukata tamaa hata kipindi cha kwanza kilipokuwa kigumu. Waliamini kwenye mpango wetu – na matokeo yanaonyesha.”
Kwa matokeo haya, Arsenal wanaendelea kuongoza kundi lao wakiwa na ushindi wa tatu mfululizo, wakitoa onyo kali kwa vigogo wa Ulaya kuwa safari yao ya kutafuta taji la Ligi ya Mabingwa ina nguvu mpya.


Napenda kurekebisha Mpira uliopigwa na Rice kwa ajili ya goli la kwanza ulikuwa ni mpira uliokufa na si kona. Otherwise kila kitu kiko salama brother. Well articulated
Ohhh, Asante sana🤝🤝🤝