in , , , ,

Tunataka Kuwa Wasindikizaji Olympiki Kila Mwaka?

Tangu nakua na kujielewa nimekua nikisikia kuhusu ushiriki wa Tanzania katika michuano ya Olimpiki kwenye vipengele mbalimbali kama vile kuogelea , masumbwi na riadha ambapo tumekua tukichuana na nchi mbalimbali.

Kupitia michuano hii ya Olimpiki basi kuna jina ambalo liliweka rekodi yake kutoka Tanzania na kutwaa medali ya fedha mwaka 1980 kwenye michuano ambayo ilifanyika nchini Urusi lakini baada ya hapo kwangu mimi nikiri kwamba nimekua mara nyingi nikiona ni kama tunaenda kuwasindikiza wenzetu na kuonekana tunashiriki na wala hatuendi kushindana.

Ili Tanzania iweze kufanya vizuri kwenye michuano ya Olimpiki, ni muhimu kuweka mikakati madhubuti katika ngazi ya kitaifa kwa kuhakikisha maandalizi ya muda mrefu na kuwekeza kwenye vipaji vya wanamichezo. Hii inahitaji juhudi kutoka serikalini, taasisi za michezo na jamii kwa ujumla.

Wakati tunapata nafasi hizi za kushiriki kwenye michuano hii ya Olimpiki kila mwaka ni wakati ambao Serikali na sekta binafsi zinapaswa kuongeza uwekezaji katika michezo kwa kutoa fedha kwa ajili ya vifaa vya kisasa, miundombinu ya mazoezi na mafunzo. Bila vifaa bora na viwanja vya kisasa, wanamichezo hawawezi kufikia viwango vya kimataifa. Uwekezaji huu unahusisha pia kutoa fedha za kutosha kwa ajili ya safari za mafunzo nje ya nchi ambako wanamichezo wanaweza kujifunza na kujiandaa katika mazingira ya kimataifa.

Lakini pia ili Tanzania iweze kupata wanamichezo bora ambao wanakua wanawakilisha nchi katika michuano ya Olimpiki ni lazima kuwe na mfumo wa kugundua na kuendeleza vipaji tangu wakiwa wadogo. Programu hizi zinaweza kuanzishwa mashuleni na kwenye jamii. Michezo inapaswa kuwa sehemu ya mtaala wa elimu ambapo walimu watasaidia kugundua watoto wenye vipaji maalum katika michezo kama riadha, ndondi, kuogelea na kadhalika. Kuweka mfumo huu utahakikisha vipaji vinaendelezwa na kuandaliwa mapema kwa mashindano ya kimataifa.

Wakati tunahangaika kutafuta uwekezaji sahihi wa michezo pamoja na kuandaa mfu,mo bora wa kugundua na kuendeleza vipaji tusikatae kuwa ubora wa kocha unaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa matokeo ya mwanamichezo. Tanzania inahitaji makocha wenye uzoefu na uwezo wa kufundisha viwango vya kimataifa. Hawa ni makocha ambao wamepitia mafunzo ya juu na wanajua mbinu za kisasa na wanaweza kusaidia wanamichezo kupambana na changamoto za kiufundi na kisaikolojia. Serikali na Shirikisho la Michezo inapaswa kushirikiana kuajiri makocha bora na kuwekeza katika kuwapa mafunzo makocha wa ndani.

Moja ya changamoto kwa wanamichezo wa Tanzania ni ukosefu wa uzoefu wa kushiriki kwenye mashindano makubwa kabla ya Olimpiki. Serikali na mashirikisho ya michezo inapaswa kuhakikisha kuwa wanamichezo wanapata fursa ya kushiriki mara kwa mara katika mashindano ya kimataifa ambayo yatawasaidia kupata uzoefu na kujiamini zaidi. Kwa njia hii, wanamichezo watazoea shinikizo la mashindano makubwa na kuboresha mbinu zao. Ndio maana tunaona katika mchezo wa mpira wa miguu unavyozidi kukua Tanzania ni kupitia mambo kama haya.

Wakati mwingine ni muhimu kuainisha michezo ambayo Tanzania ina nafasi nzuri ya kufanikiwa katika Olimpiki. Kwa mfano, Tanzania imekuwa na historia nzuri kwenye riadha, hasa mbio za masafa marefu. Kutokana na hili nadhani serikali inaweza kuweka mkazo zaidi kwenye michezo ambayo Tanzania ina nafasi nzuri, na hivyo kuongeza uwezekano wa kuleta medali.

Lishe bora na afya njema ni mambo muhimu kwa mwanamichezo yoyote. Tanzania inapaswa kuhakikisha kuwa wanamichezo wake wanapata lishe bora inayosaidia kuimarisha nguvu na stamina yao. Pia, kuwe na huduma bora za afya kwa wanamichezo ili kuepuka majeraha yasiyo ya lazima na kuwasaidia kurejea haraka pale wanapoumia. Huduma za afya ya kisaikolojia pia ni muhimu ili kuhakikisha wanamichezo wanakuwa na utulivu wa kiakili wakati wa mashindano.

Jamii inapaswa kushiriki kikamilifu katika kuhamasisha vijana kushiriki michezo na kudumisha vipaji vyao. Shirikisho la Michezo Tanzania linaweza kuanzisha programu za uhamasishaji zinazolenga kuvutia vijana wengi zaidi katika michezo. Pia, serikali na wadau wa michezo, kama vile makampuni binafsi, vyuo vikuu na vyombo vya habari, wanapaswa kushirikiana kwa karibu katika kuwaendeleza wanamichezo.

Mafanikio ya Tanzania katika Olimpiki yanahitaji mikakati endelevu inayojikita katika uwekezaji, maandalizi ya muda mrefu, na ushirikiano wa karibu kati ya wadau wote. Tanzania ina vipaji vingi ambavyo vikiendelezwa ipasavyo vinaweza kuiletea nchi sifa kubwa kimataifa. Kwa kutumia mikakati hii, Tanzania inaweza kufanikiwa na kuanza kushindana kwa ushindani mkubwa kwenye medani ya kimataifa kama Olimpiki.

ReplyForward

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0
Tanzania Sports

Yanga bila Djigui Diara itakuwaje?