MASHINDANO ya CHAN yanayoendelea yameonesha burudani ya aina yake. ufundi wa wachezaji binafsi na makocha wao ni miongoni mwa mambo yanayovutia kwenye michuano hii. Kuanzia jijini Kampala nchini Uganda, hadi Nairobi nchini Kenya na Dar Es Salaam na Zanzibar nchini Tanzania mashabiki na wadau wa soka wameshuhudia vipaji vya wachezaji mbalimbali kwenye mashindano haya. Moja ya matukio ya kukumbukwa katika mashindano ya CHAN ni namna timu wenyeji wanavyofurukuta ili kuonesha makucha yao.
Tathmini ya TANZANIASPORTS inaonesha kuwa Taifa Stars imebeba matumaini makubwa katika mashindano haya baada ya kushinda katika mchezo wa pili kwenye kundi lao. Tanzania ilishinda mchezo wa kwanza dhidi ya Barukina Faso kwa mabao 2-0, kabla ya kuibuka na ushindi mwingine 1-0 dhidi ya Mauritania. Kama kuna jambo linasisimua mashabiki wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa sasa ni namna mabao ya kiufundi yanavyofungwa.
KENYA VS DR CONGO
Augustine Odhiambo alipokea pasi akiwa kwenye kona ya mita 18 upande wa kulia. alikokota mpira ule na kuwalamba chenga wapinzani wake, kisha akapiga shuti kuelekea langoni na kutinga wavuni. Bao hilo lilikuwa la kwanza kwa Kenya katika mashindano ya CHAN mwaka huu na lilikuwa la tatu kwa wenyeji. Tanzania ilishapachika mabao mawili dhidi ya Burkina Faso hivyo Augustine Odhiambo aliandika bao la tatu kwenye mashindano, licha ya wenyeji wenza hao kucheza katika kiwango duni. Hili lilikuwa bao muhimu kwa Harambee Stars.
TANZANIA VS BURKINA FASO
Magoli mawili kutoka kwa wachezaji mapacha kwa kipindi cha miaka 10 ndani ya klabu ya Simba yameipa sifa pomoni Taifa Stars. Mohammed Hussein alipachika bao tamu katika mchezo wa ufunguzi na kuwa la pili kwa Taifa Stars.
Katika bao hilo ambalo lilimlazimisha mwamuzi wa mchezo kuwasiliana na wale wa VAR ili kujua uhalali wake. bao la Mohammed Hussein lilikuwa la video. Liandaliwa kwa ustadi kuanzia katikati ya dimba, Mohammed Hussein alipeleka pasi kwa mwenzake, kisha ikarudishwa kwenye kona ya 18, kabla ya kupelekwa wingi ya kushoto kwa Iddy Nado.
Kana kwamba haitoshi, Nado aliinua kichwa chake kutazama eneo la hatari la Burkina Faso namna walinzi walivyojipanga. Safu ya ulinzi ilitegemea krosi kubwa ya kutua kwenye boksi lao, laki Iddi Naod alikuwa na akili nyingine. Alimwangalia Mohamed Hussein aliyekuwa anakimbilia eneo la hatari. Yakafanyika mawasiliano, Mohammed Hussein akarudi nyuma hatua kama tatu hivi na kumtoroka beki aliyekuwa anajaribu kudhibiti na kuchunga nyendo zake.
Krosi fupi iliyopigwa na Nado ikatua kichwani mwa Mohammed Hussein. Jinsi alivyofunga bao lile ambalo liliashiria kuwa ni jukumu la mshambuliaji. Ufungaji wa bao hilo umezoeleka kwa washambuliaji lakini Mohammed Hussein ni beki, mzuri wa krosi, mzuri wa pasi za mwisho na mlinzi imara. Kufungwa kwa bao hilo kulileta sifa nyingi na hakika Mohammed Hussein alijiongezea sifa nyingine muhimu katika mchezo huu.
TANZANIA VS MAURITANIA
Huu ulikuwa mchezo wa pili wa mashindano ya CHAN. Shomari Kapombe ni beki wa kulia mahiri ambaye amekuwa akitamba kwa takribani miaka 10 sasa. ni maarufu kwa jina la Baba Esther. Katika mchezo huu sifa za Mohammed Hussein zilienda kwa pacha wake Shomari Kapombe.
Mpigaji wa krosi ya bao la ushindi alikuwa yuleyule aliyempigia krosi fupi Mohammed Hussein. Huyo si mwingine Iddy Nado kutoka klabu ya Azam. Wakati Mauritania wakiwa na imani ya kuibuka na pointi 1 walijikuta wanashuhudia Taifa Stars wakiwa kwenye nderemo na vifijo. Mauritania walikuwa wanahesabu dakika chache tu mpira umalizike, lakini mashambulizi kama nyuki ya Taifa Stars yaliwakosesha wageni hao alama moja. Shomari Kapo,mbe alikutana na krosi maridadi kutoka kwa Iddy Nado.
Winga huyo wa Taifa Stars alitukimbiza majalo mazuri kwenye boksi la Mauritania, ambao hawakuona namna Shomari Kapombe alivyofanya hesabu za haraka na kuingia kwenye boksi hilo, akatuliza mpira kwa mguu wa kulia kisha mguu wa kushoto ukatuma salamu za ushindi katika lango la Mauritania. Likawa bao la ushindi kwa Taifa Stars na kujikusanyia pointi 6 za mashindano.
DENI LA UGANDA
Uganda walianza mashindano haya kwa kichapo cha mabao 3-0 kutoka kwa Algeria. Hata hivyo tathmini ya TANZANIASPORTS inaonesha kuwa Uganda Cranes wana changamoto nyingi katika kikosi chao. Ili waweze kupata angalau goli la video, lazima wafanye kazi nzito kwenye mechi zao zijazo.

