ARSENAL WANANUFAIKA
SUNDERLAND — Uwanja wa Stadium of Light umeingilia tena mbio za ubingwa wa Ligi Kuu England baada ya Sunderland kuwazuia Manchester City kwa sare ya bila kufungana siku ya Mwaka Mpya.
Matokeo hayo yanawaacha mabingwa watetezi wakiwa pointi nne nyuma ya vinara Arsenal baada ya nusu ya kwanza ya msimu, huku kikosi cha Pep Guardiola kikishindwa kuvunja ngome imara ya wenyeji waliocheza kwa nidhamu, nguvu na kujituma kwa dakika 90.
Kwa mara nyingine tena, timu inayowania taji ilikutana na upinzani mkali katika uwanja huo, kama ilivyowatokea Arsenal mapema msimu huu. Sunderland waliendeleza rekodi yao ya kutopoteza nyumbani, wakionyesha kwa nini Stadium of Light imekuwa uwanja mgumu kwa wageni wote msimu huu.
ARSENAL WANACHEKA
Kwa matokeo haya, Arsenal ndio wanaoonekana kunufaika zaidi. Ushindi wao wa kishindo wa mabao 4-1 dhidi ya Aston Villa, sambamba na City, Liverpool na Chelsea kupoteza pointi, umeipa timu ya Mikel Arteta pengo la pointi nne kileleni mwa ligi.
Ingawa Guardiola angependa ushindi kamili dhidi ya timu iliyopandishwa daraja, sare hii inaweza kutazamwa kama matokeo yanayokubalika kutokana na uimara wa Sunderland nyumbani.
MAPAMBANO YA HAALAND NA MUKIELE
Mojawapo ya simulizi kubwa za mechi ilikuwa pambano kali kati ya mshambuliaji Erling Haaland na beki wa Sunderland, Nordi Mukiele. Kwa kiwango kikubwa, Mukiele alimzimisha Haaland, akitumia uzoefu wake wa soka la Ulaya kushinda mapambano ya juu, kukata pasi hatarishi na kumzuia mfungaji huyo hatari kupata nafasi nyingi.

Haaland alipata nafasi moja ya wazi kipindi cha kwanza baada ya pasi ya Phil Foden, lakini kwa ujumla City walipata mashuti mawili tu kipindi hicho — idadi ndogo zaidi kwa timu ya Guardiola msimu huu.
CITY WALIKOSA MAKALI PEMBENI
Kwa mshangao wa wengi, nguvu ya City kupitia mabeki wa pembeni haikuonekana kwa kiasi kikubwa. Nico O’Reilly na Matheus Nunes walilazimika kucheza kwa tahadhari zaidi kutokana na presha ya Sunderland, hali iliyopunguza mchango wao wa kushambulia.
Nafasi bora ya City ilitengenezwa na mchezaji wa akiba Josko Gvardiol, ambaye alilazimisha kipa Robin Roefs kufanya kazi kubwa kuokoa mpira uliokuwa unaelekea wavuni.
GUARDIOLA ARIDHIKA KIDOGO
Akizungumza baada ya mechi, Guardiola alisema anachukua pointi hiyo kwa mtazamo chanya.
“Kipindi cha pili tulicheza vizuri sana na tulitengeneza nafasi nyingi lakini tukashindwa kumalizia. Nimeridhika na kiwango cha timu, hasa baada ya mapumziko,” alisema.
Kocha huyo aliongeza kuwa matokeo haya ni ya onyo kwa timu yake kwamba katika mbio za ubingwa, makosa madogo yanaweza kugharimu, hasa wanapokutana na timu zinazocheza kwa nidhamu na kujituma kama Sunderland.
Manchester City sasa wanageuza macho yao kwenye pambano gumu dhidi ya Chelsea, huku Arsenal wakiendelea kuongoza mbio za taji la Ligi Kuu England.