UNAPOZUNGUMZIA soka la Afrika na umahiri wa nchi zake bila shaka yoyote Zambia itakuwa miongoni mwao. Labda kwa kuangalia ukanda wa Nchi za Kusini kwa Afrika, Zambia ni miongoni mwa nchi zenye ushawishi kutokana namafanikio yao. Zambia imekuwa nchi ambayo imetoa nyota wakali wa soka la Reinford Kalaba, Kalush Bwalya na wengineo. Hii sin chi yenye kutiliwa shaka kwa uwezo wake. ni nchi ambayo imepitia katika historia nzuri sana za soka.
Kuanzia kwenye mashindano ya AFCON ambako iliwahi kuwa bingwa, na miaka ya nyuma pia kufika nusu fainali na kutetemesha vigogo mbalimbali. Unapoangalia vipaji na suala la ununuzi wa wachezaji unagundua kuwa wale wanaotoka Zambia wana nafasi nzuri kununuliwa kwenye vilabu mbalimbali barani Ulaya na kwingineko. Sababu za Zambia kupewa nafasi kwa vipaji vyao inatokana na historia ya kuibua nyota wakali waliokuja kutikisa kwenye soka la ngazi ya klabu au timu za Taifa.
Hata hivyo Zambia ile iliyokuwa mahiri kwa sasa imekuwa kwenye changamoto kubwa. Katika mashindano ya CHAN yanayoendelea katika viwanja vya nchi Tatu za Kenya, Uganda na Tanzania imeonekana wazi Zamba ya sasa ni timu dhaifu mno chini ya kocha Avram Grant.
Kwanza kwa sifa zake za ukocha, Grant ni kocha anayesifika kwa mengi akiwa na uzoefu wa kufundisha kandanda sehemu mbalimbali duniani. Huyu ni kocha aliyezaliwa huko Israeli lakini akajitokeza kuwa kocha wa Chelsea wakati ikimilikiwa na Roman Abramovich. Kwahiyo Zambia wana kocha mwenye sifa za Kimataifa katika mashindano haya ya CHAN. Lakini matokeo ya Zambia kwenye mashindano ya CHAN hayaridhishi na yamesababisha mjadala mkubwa kuhusiana na nafasi yake ya ukocha katika nchi hiyo.
Akizungumza na vuombo vya habari kwenye moja ya mikutano yake ya kabla ya mchezo wa timu ya Taifa ya Zambia huko nchini Uganda, Avram Grant alibainisha kuwa Zambia imeingia kwenye mashindano ya CHAN ikiwa na malengo tofauti. Grant hakuonekana kusitikishwa na matokeo mabaya ya Zambia kwenye mashindano hayo. Bata yake aylisistiza kuwa Zambia inashiriki CHAN huku ikiwa na malengo tofauti na matarajio ya wengi. Bila shaka Grant anaiandaa Zambia ya kufuzu kwa mashindano ya AFCON mwaka 2027 wakati ambao Tanzania, Kenya na Uganda zitakuwa mwenyeji kwa mara ya kwanza ikifanya kwa ushirikiano.
Kulingana na taarifa za CAF, mashindano ya AFCON yamewahi kuandaliwa na Mataifa mawili, mfano Ghana na Nigeria mwaka 2000, na baada ya hapo hakuna nchi tatu zilizopewa uenyeji katika mashindano hayo. Hivyo basi Tanzania , Kenya na Uganda zinabaki kuwa nchi za kwanza kuandaa CHAN na AFCON mwaka 2027 kwa ushirikiano.
Wakati Mashindano yakiwa yanaandaliwa kwa jirani yake, Zambia imekuwa katika kipindi kigumu. Uchezaji wao karibu kila mechi umekuwa wa kibinafsi zaidi kuliko kutumikia mbinu za mwalimu wao. Zambia wana vipaji vingi katika kikosi chao, lakini hawana uchezaji wa kitimu hadi sasa na kulifanya taifa hilo kuwa daraja la kuchukua pointi.
Tathmini ya TANZANIASPORTS inaonesha kuwa Avram Grant huenda akawa kocha wa kwanza kufukuzwa kwenye katika timu ya Taifa kwenye mashindano ya CHAN. Kocha wa pili ni wa Nigeria ambaye timu yake imekuwa ikibugizwa mabao mengi kwenye mashindano ya CHAN yanayoendelea.
Sababu za kufukuzwa Grant zinajikita katika masuala ya ufundi, ambapo Zambia hawaonekani kuwa tishio kama ilivyo kawaida yao. Zambia ya Grant imekuwa nyepesi na inacheza bila kuwa na mpango mahsusi wa kuibuka na ushindi. Sababu hii na nyinginezo zinaweza kutumika kama njia ya kufukuzwa kwake kazi ya ukocha nchini Zambia.
Kilichobaki sasa ni kuangalia ni lini kibarua chake kitaota nyasi, ambapo itawasaidia Zambia wenyewe kupata mawazo mapya ya kiufundi kuliko kocha waliyenaye sasa ambaye anaonekana kuchoka katika usimamizi wa timu hiyo.
Je, Wazambia wapo tayari kuendelea na kocha huyo huku wakisingizia kuwa wanaandaa timu imara ya kushiriki mashindano ya AFCON mwaka 2027 kuliko kuipa kipaumbele CHAN? Hilo ni suala la kusubiri na kuona namna gani chama cha soka cha Zambia, FAZ kitakavyofanya kwa maslahi ya mashabiki wao wa soka.

