Menu
in , , ,

Thomas Tuchel na England

Mbali na Shaka za Uteuzi wake, Kuna Sababu za Matumaini kwa England

Jumatano hii, Shirikisho la Soka la England (FA) limemtangaza Mjerumani Thomas Tuchel kuwa kocha mpya wa timu ya taifa, kuchukua nafasi ya muda ya Lee Carsley. Uteuzi huu umepokelewa kwa mbwembwe, lakini pia umeibua maswali muhimu: Je, uteuzi huu unapeleka ujumbe gani kwa makocha wazawa wa England? Je, kocha mgeni ataendana na mfumo wa nchi? Na zaidi, je, Tuchel atafanikiwa kumudu shinikizo kubwa la kuleta mafanikio kwa timu ambayo mara nyingi huonekana kama imeandaliwa kushindwa?

Mapokezi yenye Shaka na Ukosoaji

Licha ya sifa zake kubwa, uteuzi wa Tuchel haujakosa kupingwa na kuibua hisia mchanganyiko. Baadhi ya wakosoaji wameanza kulalamika mara tu alipotangazwa. Danny Mills, mchezaji wa zamani wa Leeds United na England, hakuvutiwa na mavazi yake ya kawaida ya hoodie na kofia, akipendekeza kwamba Tuchel anapaswa kuvaa rasmi zaidi kwa suti, kama vile alivyokuwa Gareth Southgate. 

Gary Neville, nyota wa zamani wa Manchester United na England, anadai kuwa Tuchel hafai kulingana na “vigezo vya St George’s Park,” kitu ambacho FA kilidhamiria katika kujenga makocha wazawa. Wengine kama Scott Minto wamekatishwa tamaa kuwa Eddie Howe hakuteuliwa, huku Dean Ashton akiongeza kwamba uteuzi huu ni “wa kufadhaisha kidogo.”

Lakini hoja hizi haziegemei mantiki pekee. Badala yake, hisia za uzalendo na utambulisho wa taifa ndizo zinazochochea mjadala huu. Je, kocha wa kigeni anaweza kweli kuelewa na kumudu matarajio ya taifa hili lenye historia ndefu ya soka? Maswali haya yamekuwa sehemu ya mijadala ya uteuzi wa makocha wa kigeni, hata wakati makocha wazawa hawajapata mafanikio makubwa.

Historia ya Makocha wa Kigeni na Mafanikio ya Kimataifa


Tuchel sio kocha wa kwanza wa kigeni kupewa majukumu makubwa kama haya. Nchi kama Ufaransa, Italia, Uholanzi, Argentina, na Ureno zimewahi kuongozwa na makocha wa kigeni, na nchi kama Ugiriki, Korea Kusini, na Senegal zimeshuhudia mafanikio makubwa chini ya makocha wageni. Hata Brazil, moja ya mataifa yenye historia kubwa katika soka, walitumia miaka mingi wakimshawishi Carlo Ancelotti achukue mikoba ya kuiongoza timu yao.

Hii inadhihirisha kuwa uwepo wa kocha wa kigeni sio kikwazo kwa mafanikio ya timu ya taifa. Nchi nyingi zimefaidika kwa kuwa na kocha mwenye mtazamo mpya, huru kutokana na mizigo ya kihistoria ya nchi hiyo. Na hapa ndipo Tuchel anaweza kuwa na faida kubwa. Anaweza kuleta mtazamo tofauti na mbinu bora za kimataifa, jambo ambalo linaweza kusaidia England kufikia malengo makubwa, kama Kombe la Dunia 2026.

Changamoto ya Kukuza Makocha Wazawa


Hata hivyo, swali la mustakabali wa makocha wazawa wa England bado linaendelea kuwa muhimu. Changamoto kwa makocha wazawa ni kubwa, hasa katika soka la ngazi za juu. Liverpool hawajawahi kuwa na kocha mzawa tangu mwaka 2011, Manchester City tangu 2007, na Manchester United tangu 1986. Katika kipindi cha miaka 13 iliyopita, idadi ya makocha wazawa waliopata nafasi kubwa  na kwenye timu kubwa za England ni wawili tu: Frank Lampard na Graham Potter. Na hata hao walipata nafasi hizi katika mazingira fulanui. Chelsea walifungiwa kusajili wa wachezaji na hivyo kukosa matarajio ya moja kwa moja ya kushinda mataji makubwa.

Hii inaonyesha kuwa sio makocha wa England hawana uwezo, bali nafasi za kuthibitisha uwezo wao zimekuwa chache. Mfumo wa kutoa nafasi kwa makocha wazawa unahitaji mabadiliko ya muda mrefu, kwani vilabu vikubwa mara nyingi huwategemea makocha waliothibitisha uwezo wao kimataifa badala ya kutoa fursa kwa makocha wazawa chipukizi.

Uwezo wa Thomas Tuchel na Matarajio kwa England

Tanzania Sports
Thomas Tuchel


Tuchel anakuwa kocha wa tatu wa kigeni kuiongoza England, baada ya Sven-Göran Eriksson na Fabio Capello. Eriksson, Mswidi wa kwanza kuongoza England, aliwapeleka katika robo fainali za Kombe la Dunia la 2002 na 2006, pamoja na Euro 2004, lakini hakushinda taji lolote kubwa. Capello, kocha mwenye mafanikio makubwa kwenye vilabu, pia alishindwa kuleta taji la kimataifa, akiondoka baada ya mgogoro kuhusu nahodha wa timu, John Terry.

Sasa Tuchel anakuja akiwa na rekodi ya kushinda mataji makubwa katika vilabu kama Borussia Dortmund, PSG, Chelsea, na Bayern Munich. Akiwa PSG, Tuchel alishinda mataji sita, na alipokuwa Chelsea aliongoza timu kushinda Ligi ya Mabingwa Ulaya. Pia, akiwa Bayern Munich, alishinda Bundesliga, Super Cup ya UEFA, na Kombe la Dunia la Vilabu vya FIFA. Kwa ujumla, Tuchel ameshinda mechi 351 kati ya 613 alizoongoza, kiwango cha ushindi cha asilimia 57.26, rekodi ya kuvutia kwa kocha yeyote.

Hii inaonyesha uwezo wake wa kufanikisha malengo katika mazingira magumu. Kama alivyoelezwa na Mikel Arteta, “Yeye ni mmoja wa makocha bora zaidi duniani kwa maoni yangu, kwa jinsi anavyoiweka timu zake.” Maneno haya yanaonyesha heshima kubwa kwa Tuchel kutoka kwa wenzake. Na kama ataweza kupunguza mizigo ya kihisia na shinikizo kubwa kutoka kwa mashabiki wa England, ana nafasi ya kufanya mambo makubwa.

Licha ya changamoto zinazomkabili, Tuchel ni kocha mwenye uwezo mkubwa wa kiufundi na rekodi ya mafanikio. England, taifa lenye njaa ya taji kubwa la kimataifa kwa zaidi ya miaka 60, inaweza kuona matumaini mapya chini ya uongozi wake. Ingawa kuna njia nyingi ambazo uteuzi huu unaweza kuanguka, pia kuna nafasi moja kubwa ya mambo kwenda sawa na kuleta mafanikio makubwa. Ni wakati wa kusubiri na kuona kama Thomas Tuchel atakuwa kocha atakayevunja mwiko na kuleta furaha ya taji kwa England., lakini mafanikio yake yanaleta matumaini.

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

Leave a Reply

Exit mobile version