Menu
in

Joel Bendera apewe Taifa Stars!

Cape Verde imeifunga Tanzania 1-0 katika kundi la 1, katika kuwania kufuzu kwa mashindano ya kombe la Dunia 2010 nchini Africa kusini. Nimatokeo yasiowashangaza wengi wanaofuatilia maendeleo ya soka la Tanzania na mwalimu wa Taifa Maximo.

Huu ni ushindi wa kwanza kwa nchi hii ya Cape Verde katika mashindano haya muhimu. Matokeo yanayoiweka Cape Verde katika nafasi ya pili kandika kundi hili lenye timu za Cameroon na Mauritius pia.

Matokeo haya yanaiweka Taifa Stars katika wakati mgumu, kwani baada ya kucheza michezo miwili wanashikilia mkia wakiwa na point 1!.

Mchezaji wa akiba Babanco ndiye aliyekuwa mwiba kwa Tanzania pale alipo funga goli pekee katika mchezo huo katika dakika ya 73 ya mchezo huo, uliochezwa katika jiji la Praia.

Tanzania itakuwa na wakati mgumu sana, pale itakapo wakaribisha washindi wa pili wa kombe la mataifa ya Afrika, Cameroon katika mchezo utakaofanyika jijini Dar-es-Salaam ndani ya wiki mbili zijazo.

Kwa muda mrefu sasa mashabiki wa soka nchini Tanzania wamekuwa wakihoji uimara wa kocha Mkuu Maximo. Hii inafuatia tabia yake ya kubadili wachezaji kila mara, na hivi karibuni kulaumu aina ya wachezajia alionao, kuwa eti hawafundishiki!.

Anawalaumu kuwa hawafungi magoli pale wanapotakiwa kufunga, na kuwa sio kazi ya walimu wa Taifa kuifanya hiyo kazi, huku akiamini hiyo ni kazi ya walimu wa vilabu, nikauli isiyokuwa na maana machoni mwa wapenzi wa soka.

Serikali imetumia mamilioni ya pesa na bado inatumia pesa nyingi kuendelea kuwa na Mbrazil huyu, kwa lengo la kukuza kiwango cha soka cha Tanzania, pia kuhakikisha Tanzania inafuzu katika mashindano muhimu katika Bara la Afrika, hii ikiwa ndio sababu ya kumtafuta kocha anayetoka Taifa la soka duniani, Brazil.

Binafsi sina tatizo na Maximo, kama binadamu! ila kama mwalimu, nina wasi wasi kama anaufahamu mzuri wa aina ya soka la Afrika, Hakuna kumbukumbu zozote zinazoonyesha mafanikio kwa walimu toka Brazil katika soka la Afrika.

Mafanikio makubwa katika soka kwa baadhi ya Nchi za Afrika kama Nigeria, Togo, Senegal, Mali,Ghana, Ivory Coast bila kusahau Cameroon, yameletwa na Walimu toka Ufaransa, huu ni ukweli ulio wazi, wafaransa wanaifahamu vizuri sana soka ya Afrika, na ndio sababu nchi kama ya ufaransa ina wachezaji wengi wenye asili ya afrika, na hivyo kuzisaidia nchi za Afrika kisoka.

Kazi inayofanywa na Maximo, ingeweza kufanywa vizuri zaidi na mwalimu mzalendo kwa kumpa msaada na heshima anayopewa Maximo, huku viongozi wa serikali wakimtetea kuwa anafanya kazi nzuri kuendeleza soka na aendelee kupewa nafasi, mimi sidhani kama mafanikio aliyoyapata kwa kipindi chote alichokaa na Taifa stars, hayakuwahi kufikiwa na walimu wazalendo waliomtangulia, ila kwa kuwa ni MBRAZIL, basi chochote kidogo anachopata uwanjani kinakuzwa mara 100!

Kwa uelewa wangu kiongozi anapimwa kutokana na matokeo ya kazi yake, na ndio maana Vilabu na Nchi nyingine duniani haziishi kufanya mabadiliko katika uongozi wa soka, hasa pale matokeo yanapokuwa hayaendani na aina ya uongozi wa hizi taasisi za michezo, ambazo hugusa hisia za wananchi wake.

Kwa mtazamo wangu na ushauri wangu, ni vyema Mhe Rais Jakaya Kikwete, ampe Mhe Joel Bendera likizo fupi, ili awe mwalimu wa hii timu ya Taifa kwa kipindi kifupi kilichobakia kabla ya Tanzania kufufua matumaini yake ya kuwa moja kati ya Timu zitakazo fuzu kwenda Afrika kusini 2010.

Kwani tukumbuke Joel Bendera alikuwa ni Kocha mkuu wa Taifa Stars ya mwisho kufanya vizuri katika mashindano ya Afrika bila kusahau kule Nigeria mwaka 1980.

Huyu ni mtaalamu wa soka aliyebobea, badala ya kufundisha timu za wabunge, apewe vipindi vya kuwa na wachezaji wa Taifa Stars. Kama Mwalimu, Kocha, Mbunge na Naibu Waziri wa michezo, atasaidia kujua tatizo liko wapi na kutafuta dawa itakayomsaidia Maximo au mwalimu mwingine, kuitumia kuboresha kiwango cha Timu yetu hii ya Taifa.

Hii itasaidia kurudisha imani miongoni mwa wananchi, kuwa pamoja na serikali kumlipa mshahara Maximo, lakini bado inajali matokeo ya Stars katika jamii, na jamii inaonyesha kuchoka na kusubiri, Tanzania ni Nchi kubwa Duniani, ina historia kubwa na umaarufu mkubwa, wakati tunasifika kwa kuwa Taifa la Amani, kuwa na Kiswahili, Mlima Kilimanjaro, Mwalimu Nyerere, Mbuga za wanyama, Filbert Bayi, Juma Ikangaa na kutembelewa na viongozi wa mataifa makubwa, kuandaa mikutano mikubwa ya kimataifa, kuwa na Rais mpenda michezo na sifa kibao kwa nchi yetu, bado hatustahili kutokuwa na mchezaji hata mmoja kwenye ligi za kubwa za dunia!.

Wakati huo huo, TFF na Baraza la Michezo La Taifa, liangalie utaratibu mzuri wa kumpata Mwalimu wa Taifa, tumeona kule Mexico wiki iliyopita, kuwa walimu wa vilabu vya soka walipiga kura kura kumchagua Eric Goran-Ericsson kuwa kocha mkuu wa Timu ya Taifa, aina hii ya demokrasia na uwazi inasaidia kuweka hatima ya matokeo yeyote kwa mfumo wa kijamii kuliko taasisi moja.

Njia nyingine ni kutumia makampuni ya kimataifa ya mahusiano (PR) kutangaza na kusaili wale wote wanaotaka kuwa walimu wa Timu ya Taifa, katika hali ya utandawazi siku hizi, unanafasi nzuri ya kumpata Kocha mzuri wa Taifa kwa kuwatumia Ma-Agent wa kimataifa. na hii isiwe kwa soka tu, ila kwa michezo mingine yote, kwani Tanzania sio taifa la soka tu!

Harambee Stars, imeanza kufanya vizuri katika mashindano ya kimataifa, na hii ni baada ya kuwa na migogoro na kufungiwa na FIFA, CAF, kwa karibu miaka miwili hivi. Wanafanya vizuri kwa kutumia walimu wa nyumbani na hapa tusikosee Kenya itafuzu hata Uganda pia, kwani wenzetu wanajua tofauti ya kucheza nyumbani na ugenini. Je Dr Msolla, Mziray, Kayuni hawana nafasi tena katika soka letu?.

saria@tanzaniasports.com

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

Leave a Reply

Exit mobile version